Na Mwamvua Mwinyi, Kibaha
Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Abubakar Kunenge, ameiagiza Manispaa ya Kibaha kufanya tathmini ya mara kwa mara ya vipaumbele vya maendeleo ili kuhakikisha vinatoa matokeo chanya kwa wananchi na kuchochea maendeleo endelevu.
Aidha, ameielekeza Manispaa hiyo kuhakikisha mipango na vipaumbele vyake vinaendana na mahitaji ya wananchi pamoja na kuakisi matakwa ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Kunenge alitoa maelekezo hayo wakati wa Kikao Maalum cha Baraza la Madiwani cha kupitia Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa mwaka wa fedha 2024/2025, kilichofanyika Juni 18, 2026 katika Manispaa ya Kibaha.
“Tunapaswa kuwa na malengo yanayoakisi Dira ya Taifa 2050, Halmashauri zetu zihakikishe mipango yote inayotekelezwa inalenga kuboresha maisha ya wananchi na kuleta maendeleo ,” alieleza Kunenge.
Alifafanua Mkoa wa Pwani unaendelea kufanya vizuri katika ukusanyaji wa mapato ya ndani, ambapo lengo lilikuwa kukusanya Shilingi bilioni 88, lakini kufikia Aprili 2026 makusanyo yalikuwa yamefikia Shilingi bilioni 94, huku hadi Mei yakifikia Shilingi bilioni 114.5, sawa na asilimia 101 ya lengo.
Kunenge alibainisha kuwa Manispaa ya Kibaha imeendelea kufanya vizuri kwa kushika nafasi ya pili mkoani katika ukusanyaji wa mapato, ikiwa imekusanya zaidi ya Shilingi bilioni 26 hadi Mei mwaka huu.
Alisisitiza kuwa mafanikio katika ukusanyaji wa mapato na upatikanaji wa hati safi za ukaguzi yanapaswa kwenda sambamba na utekelezaji wa miradi yenye tija na matokeo yanayoonekana kwa wananchi.
“Hili la vipaumbele ni muhimu , sambamba na kupata hati safi za ukaguzi kunapaswa kwenda sambamba na utekelezaji wa miradi yenye tija na matokeo chanya” alibainisha.
Kwa upande wake, Mwakilishi wa CAG na Mkaguzi wa Nje wa Mkoa wa Pwani (CEA), Faith Mutune, alisema Manispaa ya Kibaha ilikuwa na hoja 23 za ukaguzi kwa mwaka wa fedha 2024/2025, ambapo hoja 18 zimefungwa na hoja tano zinaendelea kufanyiwa kazi.
Katibu Tawala wa Mkoa wa Pwani, Pili Mnyema, aliipongeza Manispaa ya Kibaha kwa mafanikio yake katika ukusanyaji wa mapato na kuhimiza juhudi zaidi za kuimarisha utendaji na usimamizi wa rasilimali za umma.
Naye Meya wa Manispaa ya Kibaha, Dkt. Nicas Mawazo, alieleza kupokea maelekezo yaliyotolewa na kuahidi kuendelea kuboresha ukusanyaji wa mapato ili kuongeza uwezo wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa manufaa ya wananchi
Mkurugenzi wa Manispaa ya Kibaha, Dkt. Rogers Shemwelekwa, alisema menejimenti itaendelea kushughulikia hoja tano zilizobaki ili kuhakikisha halmashauri inafikia viwango vya usimamizi wa fedha na utendaji.
















