
Unguja. Serikali ya imesema wananchi 3,682 wamelipwa fidia ya Sh47 bilioni katika maeneo 44 ya Unguja na Pemba waliopisha ujenzi wa miundombinu.
Hayo yameelezwa leo Mei 28, 2026 na Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Dk Khalid Salum Mohamed wakati akihitimisha mjadala wa makadirio ya mapato na matumizi ya wizara yake katika Baraza la Wawakilishi Unguja Zanzibar.
Dk Khalid alikuwa anbajibu hoja zilizotolewa na wajumbe wa Baraza wakati wanajadili hotuba bajeti ya wizara yake Mei 26, 2026, ambapo waliibua hoja za kutolipwa kwa wananchi kwenye maeneo yao.
Miongoni mwa walioibua hoja hizo ni pamoja na Mwakilishi wa Wawi, Bakar Hamad Bakar kuwa bado kuna wananchi wanadai fidia walipopisha ujenzi wa uwanaja wa ndege wa Pemba.
“Tunashukuru awamu ya kwanza wamepata, lakini kuna eneo ambalo hawakuingia awamu hii lakini kuna eneo Serikali imeshawazuia wasiendeleze na hawapo kwenye eneo la mradi.
“Amesema wananchi wanaogopa kuendeleza nyumba zao kwa sababu tayari Serikali imeenda kufanya tahmini “kwa hiyo tunataka kupata mustakabali wa wananchi hao kuwalipa baada ya kuongeza maeneo ya kupisha mradi huo.”
Mbali na hao, wawakilishi wengine walisema kuna wananchi ambao wameondolewa mazao vyao, lakini hawajalipwa fedha zao.
Akijibu hoja hizo Dk Khalid amesema hakuna mwananchi ambaye atadhulumiwa haki zake za fidia ikiwa wanastahili na Serikali ipo makini katika hilo.
“Mpaka sasa tayari wananchi 3,682 wamelipwa fidia, zaidi ya Sh47 bilioni zimetolewa katika maeneo 44 ya Unguja na Pemba,” amesema Dk Khalid.
Kwa mujibu wa Waziri huyo, Serikali inaendelea na taratibu za kulipa wale wote wanastahili kulipwa fidia katika maeneo yote ambayo kuna miradi ya maendeleo ya barabara.
Amesema “Rais (Dk Hussein Mwinyi) ameshatoa maelekezo kuhakikisha kila mwananchi analipwa na kupata stahiki zake, kwa hiyo tuwaondoe wasiwasi hakuna atakaye dhulimiwa.”













